Mhe. Rais Jakaya Mrisho Kikwete amesema sekondari zilizoanzishwa kila kata nchini ni fursa ya kihistoria ya kuleta usawa wa kweli miongoni mwa Watanzania. Aidha, amesisitiza kuwa elimu ndiyo itakuwa siri ya kweli ya mageuzi ya jamii ya Tanzania, na hivyo amewataka viongozi kulisimamia kikamilifu suala la elimu na kuhakikisha linafanikiwa, na kwamba elimu hiyo ya sekondari iliyopanuka katika miaka miwili iliyopita, ndiyo itadhibiti mwenendo mzima wa ongezako la watu nchini.
Katika hotuba yake ya karibu saa tatu kwenye ukumbi wa shughuli mbalimbali wa Hoteli ya Mkonge mjini Tanga, Rais Kikwete alieleza kufurahishwa kwake na jitihada zinazofanywa na wananchi wa Tanga chini ya uongozi wao katika kujiletea maendeleo.
Rais aliyetumia muda mwingi kuelezea umuhimu na manufaa ya elimu kwa umoja na usawa wa Watanzania, aliwaambia viongozi hao wa Mkoa wa Tanga: “Itabidi, ndugu zangu, twende shule. Huu ndiyo ukombozi wetu pekee. Sisi wa ukanda wa Pwani tumekuwa tunachezea elimu, na bado tunafanya mchezo, wakati wale waliotutangulia wanaonyesha umakini mkubwa.
Ni lazima tukimbie wakati wenzetu wanatembelea.” Alisisitiza Rais: “Kama mnavyojua, maeneo yale ambayo hayakuwa na Wamisionari ambao walivutiwa na hali ya hewa, hayakuwa na sekondari na yalibakia nyuma kielimu. Hata baada ya uhuru, sekondari zilikuwa maeneo ya mijini tu. Hapakuwapo sekondari kwenye makao makuu ya wilaya, achilia mbali vijijini.
Hali hiyo ilijenga mazingira ya watu fulani kuwa na fursa zaidi, na wengine kukosa nafasi kama hiyo.” Alisema maana kuu ya kujenga sekondari kila kata ni kutoa fursa sawa kwa Watanzania wote, siyo kwa wale tu waliokuwa na bahati ya kuwa na sekondari za Wamisionari. mfano duga ambako wamisionari hawakufika jamii itapata wapi fursa ya kupata elimu? |