JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA - OFISI YA WAZIRI MKUU - TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA      
tanga
 
     
 
     
MWENGE WAZIMWA TANGA 2008
 
Mwenge Tanga 2008 [ Nyumbani ] au
 
Utangulizi
 

MBIO za Mwenge wa Uhuru ni moja ya matukio yenye kulinda na kukuza historia ya nchi. Matukio hayo yanalenga kuwaenzi wanaharakati, viongozi na wananchi waliopigana kufa na kupona, kuhakikisha kuwa taifa linakuwa huru kabla na baada ya Uhuru mwaka 1961.

Kwa mara ya kwanza Mwenge wa Uhuru, uliwashwa juu ya kilele cha Mlima Kilimanjaro Desemba 9 mwaka 1961 na Baba wa Taifa, hayati Mwalimu Julius Nyerere. Tangu mwaka huo, serikali ikiongozwa na chama tawala cha Tanganyika African National Union (TANU) iliratibu na kuendeleza Mbio hizo za Mwenge wa Uhuru.

mfumo wa kukimbiza Mwenge wa Uhuru ulibadilishwa mwaka 1993, kutokana na mabadiliko ya kisiasa, yaliyotokea nchini mwaka 1992. Mwaka huo, nchi iliacha mfumo wa chama kimoja cha siasa na kuingia katika siasa ya vyama vingi. Kutoka mwaka huo, Mbio za Mwenge wa Uhuru zilirejeshwa chini ya utaratibu wa Serikali mwaka 1993.

Sasa ni mwaka wa 15 tangu Serikali ianze kuratibu na kusimamia mbio hizo, lengo likiwa ni kuondoa dhana ya kwamba Mwenge wa uhuru ni wa chama tawala, ambacho kwa sasa ni CCM. CCM ilizaliwa kutokana na muungano wa TANU na ASP ya Zanzibar. Huko nyuma, utaratibu wa mbio za Mwenge wa Uhuru, ulikuwa ukifanywa na Umoja wa Vijana wa CCM (UVCCM).

Mbio za Mwenge wa Uhuru hupita katika nchi, mikoa, wilaya na vitongoji mbalimbali, kwa kufuata falsafa ya Mwenge wa Uhuru, iliyoanzishwa na Mwalimu Nyerere enzi za uhai wake. Humulika palipo na giza na kwa sasa unamulika rushwa na maovu ya watendaji katika ngazi mbalimbali nchini.

Mbio za Mwenge ni kielelezo cha mshikamano Mwenge wa Uhuru umetoa mchango mkubwa katika kudumisha mshikamano wa kitaifa, amani, upendo na umoja miongoni mwa Watanzania.

Vilevile, mbio za Mwenge huo zimeweza kuleta msukumo wa pekee katika maendeleo ya Watanzania, hasa katika shughuli za kiuchumi, kijamii na kiutamaduni. Serikali imekuwa ikihamasisha wananchi na makundi mbalimbali, kuunganisha nguvu, kwa kuchangia kwa hali na mali ili kufanikisha miradi mbalimbali ya maendeleo.

Mwenge huzindua miradi ya kijamii Mbio za Mwenge wa Uhuru zimekuwa mstari wa mbele katika kuhakikisha dira ya maendeleo inapatikana, kwa kuweka nguvu kwenye mapambano dhidi ya Ukimwi na vita dhidi ya umasikini na ukosefu wa ajira kwa vijana.

Mchango wake unajidhihirisha wazi, kwani mbio hizo zimewezesha kuanzishwa kwa miradi mingi ya kijamii. Kwa mujibu wa taarifa za Wizara hiyo mwaka 1961 hadi mwaka 1998, miradi yenye thamani ya Sh bilioni 15 iliweza kuzinduliwa tofauti.

Na tangu mwaka 1998 hadi sasa, miradi mingine ya zaidi ya Sh bilioni 80 imezinduliwa. Miradi hiyo ni sekta ya afya na ujenzi wa shule, kupitia michango ya wadau, wahisani na wananchi wenyewe. Aidha, mbio hizo zimeelekeza nguvu katika Utandawazi, haki ya mtoto iliyopitishwa katika mikataba mbalimbali ya kimataifa.

Pia, mbio hizo zinahimiza umuhimu wa kudumisha amani na upendo wa kweli, vilivyoiwezesha nchi na wananchi wake kuwa ndugu. Kumekuwapo na ushirikishwaji au usawa kijinsia na uhamasishaji wa Watanzania, juu ya masuala mbalimbali ya maendeleo ya kiuchumi kijamii na kiutamaduni.

Ujumbe wa Mbio za Mwenge wa Uhuru kwa mwaka, huzingatia dira, programu, malengo, mikakati na masuala muhimu, yanayowakabili Watanzania na jamii ya Kimataifa. Mbio hizo zinaimarisha juhudi za serikali katika kufikiria nini kifanyike na kwa wakati gani kwa maslahi ya Taifa.

 
 
Mbio za Mwenge Mwaka 2008
 

Mwenge wa uhuru mwaka 2008 ulizinduliwa tarehe 29 Mei 2008 katika kijiji cha Msoga wilayani Bagamoyo Mkoa wa Pwani, kijiji alichozaliwa Rais wa awamu ya kwanza wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete na kubeba kaulimbiu ya ‘Tutunze vyanzo vya maji na tutumie maji tuliyonayo vizuri kwa maendeleo yetu na uhai wa vizazi vijavyo’.

Baada ya kuwashwa, mwenge ulianza mbio zake mkoani Pwani na ulimaliza mbio hizo Oktoba 13 katika Mkoa wa Tanga, na kuzimwa Oktoba 14 mkoani humo

Wakimbizaji wa mwenge wa Uhuru 2008, kutoka kushoto Suleiman Shauri Jecha kutoka Kusini Unguja, Mohamed Magati wa Pwani, Elizabeth Kalonga wa Mwanza, Kiongozi wa Mbio hizo Shames Martin Nungu wa Songea, Bakia Abdalah wa Pemba na Jeremiah Ouko kutoka Tanga wakiwa katika picha ya pamoja
 
 
 
Sherehe za kuzima mwenge wa Uhuru Mkoani Tanga Oktoba 14, 2008
 

Sherehe za kumbukumbu ya Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere hufanyika kila mwaka ambapo shughuli kadhaa zitafanyika, ikiwamo kuhitimishwa kwa mbio za Mwenge wa Uhuru. Mwenge wa Uhuru ambao ulianza mbio zake mwezi Mei mkoa wa Pwani, mwaka huu utazimwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Jakaya Mrisho Kikwete katika Uwanja wa Mkwakwani Jijini Tanga

Mwenge Tanga
 
Kabla ya kwenda kwenye uwanja huo, Rais alihudhuria ibada ya kumbukumbu ya kifo cha Mwalimu kwenye Kanisa Kuu la Mt Anthony na baadaye alitembelea maonyesho ya vijana kwenye viwanja vya Tangamano Jijini Tanga.kifo cha Baba wa Taifa ni pengo lisilozibika, lakini ni urithi mzuri wa Taifa hili kwa vizazi vijavyo.
 
Akihutubia katika sherehe hizo Rais Jakaya Kikwete alisema Shughuli za mwenge zimekabidhiwa kwa vijana kwa sababu wao ndio tegemeo la taifa la KESHO na KESHOKUTWA. Anayemkumbuka Nyerere. Ili kumkumbuka Nyerere ni wajibu wa kila mmoja kuonyesha kwa vitendo aliyoyasimamia Mwalimu. Kuhimiza upendo na kuepuka mambo yanayoleta chuki na utengano katika jamii.
 
Rais alizungumzia juhudi za serikali kukabiliana na msukosuko wa kifedha duniani. Pia alizungumza juu ya urejeshaji wa fedha za Tanzania zilizopo katika mabenki ya biashara
 
Baada ya Sherehe hizo Rais Jakaya Mrisho Kikwete alipata fursa ya kutembelea Hospital ya Mkoa (Bombo) na kufungua rasmi ujenzi wa Kiwanda kipya cha Saruji mkoani Tanga
Kiongozi wa mbio za Mwenge kitaifa Shanes Martin Nungu akikabidhi Mwenge wa Uhuru kwa Rais Jakaya Mrisho Kikwete katika uwanja wa michezo wa Mkwakwani Tanga wakati wa kilele cha sherehe za kumbukumbu ya Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere Oktoba 14, 2008

 

 

Kiwanda kipya cha Saruji chaanza kujengwa Tanga

 

Ujenzi huo umeanzishwa na Rais Jakaya Mrisho Kikwete katika sherehe ya uwekaji jiwe la msingi la ujenzi wa kiwanda hicho kitakachoanza uzalishaji Oktoba, 2010, na kuwa na uwezo wa kuzalisha tani 4,000 kwa siku. Ujenzi huo utachukua miezi 24.

Kiwanda hicho kinajengwa na Kampuni ya Athi River Mining Ltd (ARM) yenye makao yake nchini Kenya, na kitakuwa kiwanda kikubwa zaidi kuliko kingine chochote cha uzalishaji saruji katika eneo la Mashariki mwa Afrika kikiwa na uwezo wa kuzalisha tani 1,500,000 kwa mwaka.

Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni hiyo, Pradeep Paunrana amemwambia Rais Kikwete kwenye sherehe hiyo:
“Kupitia uzalishaji huu wa tani 4,000 kwa siku, tunapenda kukuhakikishia kwamba uhaba wa saruji litakuwa ni historia, bei zitakuwa za ushindani na zitakuwa bei halisi badala ya bei za sasa za saruji zinazoongozwa na uhaba wa bidhaa hiyo.”

Mkurugenzi huyo amesema kuwa kampuni yake ambayo imekuwa na shughuli nchini kwa miaka sita iliyopita, imevutiwa kuwekeza zaidi katika uchumi wa Tanzania kutokana na kugundua mvuto wa uchumi huo.

“Mheshimiwa Rais, baada ya kuwa tumeonja utamu wa uchumi wa Tanzania, na maisha yanayozidi kuwa bora kila siku kwa kila Mtanzania, lilikuwa ni jambo la dhahiri kabisa kuingia katika uzalishaji wa saruji hapa nchini,” amesema Praunrana.

ARM ambacho kwa miaka sita iliyopita imekuwa inazalisha chokaa inayotumiwa katika uchimbaji madini nchini, inazalisha bidhaa za viwandani katika Afrika Kusini, Zambia na Kenya, ambapo kampuni hiyo pia inazalisha saruji.

Mkurugenzi huyo amemwambia Rais Kikwete kuwa ARM imeamua kuwa uzalishaji wote wa siku ya kwanza Oktoba 2010, yaani tani 4,000 ama malori 125 ya saruji, itatolewa yote kwa Rais Kikwete ambaye ataamua kuitumia atakavyo kwa miradi ya kijamii aitakayo.

Kiwanda hicho kipya kitaifanya Tanzania kuwa nchi pekee katika ukanda wa Mashariki mwa Afrika kuwa na viwanda vinne vya saruji.

Viwanda vitatu vilivyoko kwa sasa ni Tanzania Portland Cement Company (TPCC) ama Twiga Cement cha Dar Es Salaam, Simba Cement cha Tanga na Mbeya Cement cha Mbeya. TPCC ndiyo kiwanda cha kwanza cha saruji Tanzania kilichofunguliwa Agosti 8, mwaka 1966 na Baba wa Taifa, Mwalimu JK Nyerere.

Akizungumza kwenye sherehe hiyo Rais Kikwete ameipongeza ARM kwa uamuzi wake wa kuwekeza katika uzalishaji wa saruji ambao sasa utaiwezesha Tanzania kuzalisha tani 3,000,000 kwa mwaka baada ya kuwa kiwanda hicho kimekamilika katika miaka miwili ijayo.
Pamoja na kwamba uzalishaji saruji nchini umekuwa unaongezeka, bado uwiano wa saruji na idadi ya wananchi wa Tanzania umebakia ndogo.

Amesema kuwa mwaka 2005 wakati wananchi wa Tanzania wanakadiriwa kufikia milioni 37, matumizi ya saruji yalikuwa sawa na kilo 37 kwa kila Mtanzania kwa mwaka.

“Matumizi haya bado ni madogo ikilinganishwa na matumizi ya saruji nchini Kenya ambayo ni wastani wa kilo 56 kwa mtu mmoja kwa mwaka. Nchini Afrika Kusini, matumizi haya yanafikia wastani wa kilo 400 kwa mtu mmoja kwa mwaka.”

 

Rais Jakaya Kikwetena Mkurugenzi wa kampuni ya ARM wakati wa kuzindua ujenzi wa kiwanda hicho Oktoba 2008, wengine ni Mkuu wa Mkoa wa Tanga Mohamed Abdulaziz na viongozi wa juu wa kampuni ya ARM

Vifaa vya Kiwanda cha Cement kipya vimewasili eneo la Ujenzi Maweni Mkoani Tangaf (4000 tpd Cement plant)
 
 
Mwenge 2008 [ Nyumbani ] au
Rudi juu
 
     
Copyright © 2008 - Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Tanga, Box 5095 Tanga, TEL: 027 - 2642430, FAX: 027-2647752